Sunday, November 4, 2012

8:10 AM
Mabao kutoka kwa straika wa kimataifa wa Burundi, Didier Kavumbagu na straika wa Uganda, Hamis Kiiza yaliipandisha Yanga kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya kuibuka na ushindi 'mtamu' wa mabao 2-0 dhidi ya Azam kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam huku mahasimu wao wa jadi, Simba wakipata kipigo cha ugenini cha 2-0 kutoka kwa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro leo.

Kama ilivyokuwa kwa Yanga, Mtibwa walifunga mabao yao pia katika kila kipindi kupitia kwa mastraika wao nyota, Said Mkopi na Hussein Javu ambaye aliwahi pia kuiliza Yanga kwa kupiga 'hat-trick' wakati 'Wanajangwani' walipolala3-0 katika mechi yao ya raundi za mwanzo wa msimu.

Katika mechi ya Taifa, Yanga walionyesha soka safi kuanzia mwanzo wa mechi hadi mwisho, wakigongeana pasi za kuvutia na kutawala mno katika eneo la katikati ya dimba lililokuwa chini ya himaya ya kiungo wao wa kimataifa kutoka Rwanda, Haruna Niyonzima 'Fabregas'.

Kavumbagu aliifungia Yanga bao la utangulizi katika kipindi cha kwanza na Kiiza alifunga goli la pili lkatika kipindi cha pili ambacho Azam walijikuta wakiusaka mpira kwa tochi kutokana na 'gonga' za kusisimua za Yanga; zikiwamo zilizozaa bao la Kiiza baada ya Fabregas, Kiiza na Chuji kupigiana 'one-two' kabla mfungaji kukwamisha mpira wavuni.

Matokeo ya mechi za leo yameifanya Yanga ikwee rasmi kileleni mwa msimamo wa ligi kuu ya Bara kwa mara ya kwanza msimu huu, ikifikisha pointi 26 na kuwaacha mahasimu wao wa jadi, Simba wanaoshika nafasi ya pili kwa tofauti ya pointi tatu. Azam inaendelea kubaki katika katika nafasi yake ya tatu ikiwa na pointi 21.

Kipigo cha leo kwa Simba inayoonekana kama ilitangulia na "baiskeli ya barafu" ni muendelezo wa matokeo mabaya kwa 'wekundu' hao, hasa katika mechi zao za ugenini kwani licha ya kuongoza kwa muda mrefu kutokana na ushindi mfululizo wa mechi zao nyingi za nyumbani; mabingwa hao watetezi walijikuta wakishikiliwa kwa sare dhidi ya Coastal Union na Mgambo JKT za Tanga, Kagera Sugar waliyocheza nayo kwenye Uwanja wa Taifa na pia wakasimamishwa kwa sare ya ugenini pia kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro dhidi ya 'maafande' wa Polisi Moro ambao ndiyo wanaoburuta mkia kwenye msimamo wa ligi hiyo.

0 comment.:

Post a Comment