Friday, November 2, 2012

3:01 PM

MENEJA Mkuu wa klabu ya African Lyon ya Dar es Salaam, inayoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Rahim Kangezi ‘Zamunda’ kesho anatarajiwa kuchukua fomu za kuwania nafasi ya Ukatibu Mkuu wa Chama cha Soka Dar es Salaam (DRFA).
Zamunda kama atachukua fomu hiyo kesho, ina maana mpinzani wake mkuu atakuwa Katibu wa sasa wa DRFA, Msanifu Kondo, ambaye amejijengea ngome imara katika kampeni kwa muda mrefu.
Akizungumza na  Fzakar.blogspot.com mida hii, Zamunda amesema kwamba awali nia yake ilikuwa kuchukua fomu ya kugombea Uenyekiti, lakini ameona tayari wamekwishajitokeza watu wenye sifa, hivyo anahamia kwenye Ukatibu.
“Mimi ni mtendaji mzuri hakuna shaka katika hilo, watu wameona nilipoitoa African Lyon hadi nilipoifikisha, nimewasaidia wachezaji wengi wa Tanzania kwenda Amerika na Ulaya kucheza soka ya kulipwa,”.
“Nimekuwa mwanaharakati wa haki za klabu za Ligi Kuu na kwa kiasi kikubwa hadi kufikia hapa klabu zinaelekea kujikomboa, kuna mchango wangu mkubwa. Sasa nataka niingie DRFA kufanya mapinduzi makubwa ya kimaendelea ya mpira na uchumi.”.
“Nataka DRFA isiwe tu ya kutegemea migawo ya mapato ya milangoni kutoka TFF, bali iwe na uwezo wake wa kujitegemea na kujiendesha. Iwe na wafadhili wa maana na wadhamini, tena kwa mikataba ya maandishi,”alisema Zamunda na kuongeza.
“Nataka nifanye mapinduzi makubwa katika soka Dar es Salaam, kampuni kubwa itakuwa mdhamini wa DRFA, klabu na wadau wa soka Dar es Salaam watanufaika sana, wachezaji wa Dar es Salaam watanufaika sana,”alisema.
Zamunda ndiye aliyempatia Nizar Khalfan nafasi ya kucheza Ligi Kuu ya Marekani, ambako alichezea klabu ya Vancouver Whitecaps na baadaye Philadelphia Union kabla ya kurejea nyumbani.
Akiwa huko, Nizar alipata fursa ya kuichezea Vancouver dhidi ya timu kadhaa za Ligi Kuu ya England, ikiwemo dhidi ya Manchester City mwaka juzi katika michezo ya kirafiki.
Zamunda pia alimpatia Mrisho Ngassa nafasi ya kwenda kufanya majaribio Seattle Sounders ya Marekani ambako alipewa nafasi ya kucheza mechi dhidi ya Manchester United mwaka juzi pia.
Mchakato wa uchaguzi wa DRFA unazidi kupamba moto na katika nafasi ya Uenyekiti, Ahmad Seif Hemed anachuana na Salum Mkemi, Evans Aveva, Ayoub Nyenzi, Juma Jabir na Meba Ramadhan, ambao ndio pekee hadi sasa wamechukua fomu.
Wagombea wengine waliochukua fomu hadi jana ni Ally Mayay, nafasi ya Makamu Mwenyekiti, Said Tuliy, Hamisi Ambari, ambao wanawania nafasi ya Ukatibu Mkuu, Shaffi Dauda na Muhisn Balhabou, Ujumbe wa Mkutano Mkuu, Shaaban Mohamed, Andrew Tupa, Siza Abdallah Chenje, Sunday Mwanahewa na Lameck Nyambaya Ujumbe wa kamati ya Utendaji na Philemon Ntahilaja, Mwakilishi wa Klabu.
Uchaguzi wa DRFA utafanyika Desemba 8, mwaka huu na fomu za kugombea nafasi mbalimbali zilianza kutolewa tangu Oktoba 29, wakati Novemba 4 hadi 8, Kamati ya Uchaguzi, chini ya Mwenyekiti wake, Juma Simba itapitia fomu za walioomba uongozi.
Novemba 9 hadi 13 utakuwa muda wa pingamizi kwa wagombea, ambazo zitajadiliwa Novemba 14 hadi 16, wakati Novemba 17 hadi 19 watatoa fursa ya kukata rufaa, ambazo zitasikilziwa Novemba 20 hadi 24 na baada ya hapo, Novemba 25 yatatangazwa majina ya wagombea waliopitishwa.
Uchaguzi wa DRFA utafanyika siku chache tu kabla ya uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), mwishoni mwa Desemba, mwaka huu.   

0 comment.:

Post a Comment